Saturday, December 19, 2015

WATUMISHI TANESCO 10 WASIMAMISHWA KAZI

Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme (Tanesco), Felchesmi Mramba, amewasimamisha kazi maofisa 10 wakiwamo wahasibu waandamizi na mafundi kwa kusababisha upotevu wa mapato zaidi ya Sh.milioni 100.


Hasara hiyo ilitokea katika mfumo wa mita kupitia minara ya simu za mkononi na faini Sh. milioni 198.1 za wateja waliobainika kuiba umeme kwa 

kuchakachua mita zao.
Hata hivyo, shirika hilo limefanikiwa kuokoa fedha hizo zilizotokana na umeme wenye thamani ya Sh. 100,248,386.42 uliotumika bila kulipiwa pamoja na faini kutoka kwa wateja waliojihusisha na wizi wa umeme Sh.
198,105,928.68.
Kadhalika, shirika baada ya kufanya msako mkali limefanikiwa kukamata taasisi binafsi na za serikali pamoja na watu binafsi wakijihusisha na kuhujumu shirika hilo,ikiwemo Shule ya Sekondari ya Jangwani (Sh. 11,023,238.00), Diwani wa Kata ya Sinza C, Joseph Marandu (Sh. 3,443,555.00), Royal Oven Bakery Kawe, (Sh. 4,112,614.00), Havan Hotel, Mbezi Beach (Sh.1,847,913.00) na Kampuni ya Simu ya Viettel Mtwara (Sh. 524,554.76).
Wengine ni, Kampuni ya Saffa Petroleum ya Mkoani Pwani (Sh. 16,105,235.00), Msanii wa Filamu Nchini, Wema Sepetu (Sh. 8,200,496.20) na Kampuni ya Leadcom (Sh. 13,694,632.81).
“Zoezi hili ni endelevu kwa nchi nzima na tutaendelea kuwakamata, kuwatangaza na kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria wale watakaobainikiwa kulihujumu shirika hatutaogopa wadhifa wala umaarufu wa mtu ama taasisi” alisema Mramba katika mkutano wake na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam.
Alisema mapema Desemba 6, mwaka huu alitoa taarifa kwa wale wote wanaojihusisha na wizi wa umeme ama wenye mita zenye matatizo, lakini walijisalimisha ni watu 30 na kati ya watu 2,156 waliokaguliwa 138 walikutwa na dosari mbalimbali katika mita zao na walilipishwa faini.
Akifafanua, alisema fedha zinazotakiwa kulipwa ni Sh. milioni 198.1 na zilizokwishalipwa ni Sh. milioni 44.9 wakati waliofikishwa kwenye vyombo vya sheria ni watu 37 kwa makosa mbalimbali. Akizungumzia kuhusu hatua atakazowachukulia watumishi 10 aliowasimamisha kazi, Mramba alisema uchunguzi unaendelea na fedha wanazodaiwa kuzifanyia udanganyifu zitalipwa na kampuni ya simu husika.
Mramba alisema ili kuhakikisha kero za huduma zinamalizika, katika kila ofisi ya kitengo cha dharula kutakuwa na  Ofisa wa huduma kwa wateja na mhandisi ambao watasimamia muda na ubora wa huduma wanazopata wateja baada ya kutoa taarida za dharura.
“Kuanzia sasa kazi ya mafundi inapokamilika maofisa hawa niliowataja watawajibika kuwapigia simu wateja waliotoa taarifa kuhakiki kama kazi zimefanywa kwa wakati na mteja ameridhika … utaratibu huu utaanza leo (jana),” alisema Mramba.

No comments:

Post a Comment